Agano la Kale

Agano Jipya

Mathayo 17:4-17 Biblia Habari Njema (BHN)

4. Hapo Petro akamwambia Yesu, “Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa! Ukipenda nitajenga vibanda vitatu: Kimoja chako, kimoja cha Mose na kimoja cha Elia.”

5. Alipokuwa bado anasema hivyo, wingu jeupe likawafunika, na sauti ikasikika kutoka hilo wingu: “Huyu ni Mwanangu mpendwa, ninayependezwa naye, msikilizeni.”

6. Wanafunzi waliposikia hivyo wakaanguka kifudifudi, wakaogopa sana.

7. Yesu akawaendea, akawagusa, akasema, “Simameni, msiogope!”

8. Walipoangalia juu hawakumwona mtu, ila Yesu peke yake.

9. Basi, walipokuwa wanashuka mlimani, Yesu akawaonya: “Msimwambie mtu mambo mliyoyaona mpaka Mwana wa Mtu atakapofufuliwa kutoka wafu.”

10. Kisha wanafunzi wakamwuliza, “Mbona waalimu wa sheria wanasema ni lazima kwanza Elia aje?”

11. Yesu akawajibu, “Kweli, Elia atakuja kutayarisha mambo yote.

12. Lakini nawaambieni, Elia amekwisha kuja nao hawakumtambua, bali walimtendea jinsi walivyotaka. Mwana wa Mtu atateswa vivyo hivyo mikononi mwao.”

13. Hapo hao wanafunzi wakafahamu kwamba alikuwa akiwaambia juu ya Yohane Mbatizaji.

14. Walipoufikia tena ule umati wa watu, mtu mmoja alimwendea Yesu, akampigia magoti,

15. akasema, “Bwana, mwonee huruma mwanangu kwa kuwa ana kifafa, tena anateseka sana; mara nyingi yeye huanguka motoni na majini.

16. Nilimleta kwa wanafunzi wako lakini hawakuweza kumponya.”

17. Yesu akajibu, “Enyi kizazi kisicho na imani, kilichopotoka! Nitakaa nanyi mpaka lini? Nitawavumilia nyinyi mpaka lini? Mleteni hapa huyo mtoto.”

Kusoma sura kamili Mathayo 17