Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13

Agano la Kale

Agano Jipya

Waebrania 5 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Kila kuhani mkuu ambaye huchaguliwa miongoni mwa watu hupewa jukumu la kushughulikia mambo ya Mungu kwa niaba ya watu, kutolea zawadi na tambiko kwa ajili ya dhambi.

2. Maadamu yeye mwenyewe ni dhaifu, anaweza kuwatendea kwa huruma wale wasiojua kitu na wanaofanya makosa.

3. Kwa sababu hiyo anapaswa kutoa tambiko si tu kwa ajili ya watu, bali pia kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe.

4. Hakuna mtu awezaye kujifanya mwenyewe kuwa kuhani mkuu. Kila mmoja huteuliwa na Mungu kuwa kuhani mkuu kama alivyokuwa Aroni.

5. Hali kadhalika naye Kristo; yeye hakujitwalia mwenyewe heshima ya kuwa kuhani mkuu, bali Mungu alimteua na kumwambia:“Wewe ni Mwanangu;mimi leo nimekuwa baba yako.”

6. Alisema pia mahali pengine:“Wewe ni kuhani milele,kwa utaratibu wa ukuhani wa Melkisedeki.”

7. Yesu alipokuwa anaishi hapa duniani, kwa kilio kikuu na machozi, alisali na kumwomba Mungu ambaye alikuwa na uwezo wa kumwokoa kifoni; naye alisikilizwa kwa sababu ya kumcha Mungu.

8. Lakini, ingawa alikuwa Mwana wa Mungu, alijifunza kutii kwa njia ya mateso.

9. Na alipofanywa mkamilifu, akawa chanzo cha wokovu wa milele kwa wote wanaomtii,

10. naye Mungu akamteua kuwa kuhani mkuu kwa utaratibu wa ukuhani wa Melkisedeki.

Onyo kuhusu uasi

11. Tunayo mengi ya kusema juu ya jambo hili, lakini ni vigumu kuwaelezeni, kwa sababu nyinyi si wepesi wa kuelewa.

12. Kwa wakati huu nyinyi mngalipaswa kuwa waalimu tayari, lakini mnahitaji bado mtu wa kuwafundisheni mafundisho ya mwanzo juu ya neno la Mungu. Mnahitaji maziwa badala ya chakula kigumu.

13. Kila anayepaswa kunywa maziwa ni mtoto bado, hajui uadilifu ni nini.

14. Lakini chakula kigumu ni kwa ajili ya watu waliokomaa, waliofunzwa kwa vitendo kubainisha mema na mabaya.