Agano la Kale

Agano Jipya

Walawi 13:43-54 Biblia Habari Njema (BHN)

43. Kuhani atamwangalia. Iwapo kuhani ataona kuwa huo uvimbe ni mwekundu-mweupe kwenye upara au kwenye paji lake na unaonekana kama ukoma kwenye ngozi yake,

44. basi, mtu huyo ana ukoma; yeye ni najisi. Kuhani atamtangaza mtu huyo kuwa najisi. Ugonjwa wake upo kwenye kichwa chake.

45. “Mwenye ukoma yeyote atavaa nguo zilizochanika, nywele zake hatazichana, na mdomo wake wa juu ataufunika na atapaza sauti akisema, ‘Mimi ni najisi, mimi ni najisi.’

46. Ataendelea kuwa najisi kwa muda wote alio na ugonjwa huo. Yeye ni najisi; naye atakaa peke yake nje ya kambi.”

47. “Kama kuna namna ya upele wa ukoma kwenye vazi, liwe la sufu au kitani,

48. vazi hilo liwe limefumwa au limesokotwa kwa kitani au sufu au ni vazi la ngozi ya aina yoyote ile,

49. iwapo upele huo una rangi ya kijani au nyekundu katika vazi hilo, basi, vazi hilo lina upele. Kwa hiyo ni lazima kumwonesha kuhani.

50. Kuhani atauangalia upele huo na kuliweka vazi hilo kando kwa muda wa siku saba.

51. Siku ya saba atauangalia upele huo. Ikiwa upele huo umeenea katika vazi hilo, liwe ni la kufuma au kusokotwa au la ngozi au la ngozi ya aina yoyote ile, vazi hilo lina upele. Hivyo vazi hilo ni najisi.

52. Kuhani atalichoma moto vazi hilo kwani lina namna ya upele wa ukoma.

53. “Kama kuhani ataona kuwa upele haukuenea katika vazi, basi,

54. ataamuru vazi hilo lifuliwe na kuwekwa kando kwa muda mwingine wa siku saba.

Kusoma sura kamili Walawi 13