Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24
  25. 25
  26. 26
  27. 27
  28. 28

Agano la Kale

Agano Jipya

Mathayo 13 Biblia Habari Njema (BHN)

Mfano wa mpanzi

1. Siku hiyohiyo, Yesu alitoka katika ile nyumba, akaenda na kuketi kando ya ziwa.

2. Makundi makubwa ya watu yalimzunguka hata Yesu akapanda mashuani, akaketi. Watu wote walisimama kwenye ukingo wa ziwa,

3. naye Yesu akawaambia mambo mengi kwa mifano.“Sikilizeni! Mpanzi alikwenda kupanda mbegu.

4. Alipokuwa akipanda mbegu, nyingine zilianguka njiani, ndege wakaja wakazila.

5. Nyingine zilianguka penye mawe pasipokuwa na udongo mwingi. Zikaota mara kwa kuwa udongo haukuwa na kina.

6. Jua lilipochomoza, ziliteketea; na kwa kuwa mizizi yake haikuwa na nguvu, zikanyauka.

7. Nyingine zilianguka kwenye miti ya miiba, nayo ikakua na kuzisonga.

8. Nyingine zilianguka penye udongo mzuri, zikaota, zikazaa: Nyingine punje mia, nyingine sitini na nyingine thelathini.

9. Mwenye masikio na asikie!”

Shabaha ya kusema kwa mifano

10. Wanafunzi wake wakamwendea, wakamwuliza, “Kwa nini unasema na watu kwa mifano?”

11. Yesu akawajibu, “Nyinyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, lakini wao hawakujaliwa.

12. Maana, aliye na kitu atapewa na kuzidishiwa; lakini yule asiye na kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.

13. Ndio maana ninasema nao kwa mifano, kwa sababu wanatazama lakini hawaoni, wanasikiliza lakini hawasikii, wala hawaelewi.

14. Kwao yametimia yale aliyosema nabii Isaya:‘Kusikia mtasikia, lakini hamtaelewa.Kutazama mtatazama, lakini hamtaona.

15. Maana akili za watu hawa zimepumbaa,wameyaziba masikio yao,wameyafumba macho yao.La sivyo, wangeona kwa macho yao,wangesikia kwa masikio yao,wangeelewa kwa akili zao,na kunigeukia, asema Bwana,nami ningewaponya.’

16. “Lakini heri yenu nyinyi, maana macho yenu yanaona na masikio yenu yanasikia.

17. Kweli nawaambieni, manabii na watu wengi wema walitamani kuyaona yale mnayoyaona, wasiyaone, na kuyasikia yale mnayoyasikia, wasiyasikie.

Maelezo ya mfano wa mpanzi

18. “Basi, nyinyi sikilizeni maana ya mfano huo wa mpanzi.

19. Yeyote asikiaye neno juu ya ufalme wa Mungu bila kuelewa, ni kama zile mbegu zilizoanguka njiani; yule Mwovu huja na kunyakua kile kilichopandwa moyoni mwake.

20. Ile mbegu iliyopandwa penye mawe ni mfano wa mtu asikiaye neno hilo na mara akalipokea kwa furaha.

21. Lakini halishiki na mizizi ndani yake; huendelea kulizingatia neno hilo kwa kitambo tu, na wakati taabu au udhalimu vinapotokea kwa sababu ya neno hilo, anakata tamaa mara.

22. Ile mbegu iliyoanguka kati ya miti ya miiba, ni mfano wa mtu asikiaye hilo neno, lakini wasiwasi wa ulimwengu huu na anasa za mali hulisonga neno hilo, naye hazai matunda.

23. Ile mbegu iliyopandwa katika udongo mzuri ni mfano wa mtu asikiaye neno hilo na kuelewa, naye huzaa matunda; mmoja mia, mwingine sitini na mwingine thelathini.”

Mfano wa magugu

24. Yesu akawaambia watu mfano mwingine: “Ufalme wa mbinguni unafanana na mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake.

25. Lakini watu wakiwa wamelala, adui yake akaja, akapanda magugu kati ya ngano, akaenda zake.

26. Basi, mimea ilipoota na kuanza kuchanua, magugu pia yakaanza kuonekana.

27. Watumishi wa yule mwenye shamba wakamwendea, wakamwambia, ‘Bwana, bila shaka ulipanda mbegu nzuri katika shamba lako. Sasa magugu yametoka wapi?’

28. Yeye akawajibu, ‘Adui ndiye aliyefanya hivyo’. Basi, watumishi wake wakamwuliza, ‘Je, unataka twende tukayangoe?’

29. Naye akawajibu, ‘La, msije labda mnapokusanya magugu, mkangoa na ngano pia.

30. Acheni vikue pamoja mpaka wakati wa mavuno. Wakati huo nitawaambia wavunaji: Kusanyeni kwanza magugu mkayafunge mafungumafungu ya kuchomwa. Lakini ngano ikusanyeni mkaiweke ghalani mwangu.’”

Mfano wa mbegu ya haradali

31. Yesu akawaambia watu mfano mwingine: “Ufalme wa mbinguni unafanana na mbegu ya haradali aliyotwaa mtu mmoja, akaipanda katika shamba lake.

32. Yenyewe ni ndogo kuliko mbegu zote, lakini ikisha ota huwa kubwa kuliko mimea yote. Hukua ikawa mti, hata ndege wa angani huja na kujenga viota katika matawi yake.”

Mfano wa chachu

33. Yesu akawaambia mfano mwingine: “Ufalme wa mbinguni umefanana na chachu aliyotwaa mama mmoja, akaichanganya na unga madebe mawili na nusu, hata unga wote ukaumuka.”

Kutumia mifano

34. Yesu aliwaambia watu hayo yote kwa mifano. Hakuwaambia chochote bila kutumia mifano,

35. ili jambo lililonenwa na nabii litimie:“Nitasema nao kwa mifano;nitafichua yaliyofichika tangu kuumbwa ulimwengu.”

Yesu anafafanua mfano wa magugu

36. Kisha Yesu aliwaaga wale watu, akaingia nyumbani. Wanafunzi wake wakamwendea, wakamwambia, “Tufafanulie ule mfano wa magugu shambani.”

37. Yesu akawaambia, “Mpanzi wa zile mbegu nzuri ni Mwana wa Mtu.

38. Lile shamba ni ulimwengu. Zile mbegu nzuri ni watu wale ambao ufalme ni wao. Lakini yale magugu ni wale watu wa yule Mwovu.

39. Adui aliyepanda yale magugu ni Ibilisi. Mavuno ni mwisho wa nyakati na wavunaji ni malaika.

40. Kama vile magugu yanavyokusanywa na kuchomwa moto, ndivyo itakavyokuwa mwishoni mwa nyakati;

41. Mwana wa Mtu atawatuma malaika wake wawakusanye kutoka katika ufalme wake wale wote wenye kusababisha dhambi, na wote wenye kutenda maovu,

42. na kuwatupa katika tanuri ya moto, na huko watalia na kusaga meno.

43. Kisha, wale wema watangara kama jua katika ufalme wa Baba yao. Mwenye masikio na asikie!

Mfano wa hazina iliyofichika

44. “Ufalme wa mbinguni unafanana na hazina iliyofichika shambani. Mtu mmoja aliigundua, akaificha tena. Alifurahi sana hata akaenda kuuza yote aliyokuwa nayo, akalinunua shamba lile.

Mfano wa lulu

45. “Tena, ufalme wa mbinguni unafanana na mfanyabiashara mmoja mwenye kutafuta lulu nzuri.

46. Alipopata lulu moja ya thamani kubwa, alikwenda, akauza yote aliyokuwa nayo, akainunua lulu ile.

Mfano wa wavu wa samaki

47. “Tena, ufalme wa mbinguni unafanana na wavu uliotupwa baharini, ukanasa samaki wa kila aina.

48. Ulipojaa, watu waliuvuta pwani, wakaketi, wakachagua samaki wazuri wakawaweka ndani ya vikapu vyao, na wabaya wakawatupa.

49. Ndivyo itakavyokuwa mwishoni mwa nyakati: Malaika watatokea, watawatenganisha watu wabaya na watu wema,

50. na kuwatupa hao wabaya katika tanuri ya moto. Huko watalia na kusaga meno.”

Hazina mpya na ya kale

51. Yesu akawauliza, “Je, mmeelewa mambo haya yote?” Wakamjibu, “Naam.”

52. Naye akawaambia, “Hivyo basi, kila mwalimu wa sheria anayekuwa mwanafunzi wa ufalme wa mbinguni anafanana na mwenye nyumba atoaye katika hazina yake vitu vipya na vya kale.”

Yesu anakataliwa huko Nazareti

53. Yesu alipomaliza kusema mifano hiyo alitoka mahali hapo,

54. akaenda kijijini kwake. Huko akawa anawafundisha watu katika sunagogi lao hata wakashangaa, wakasema, “Huyu amepata wapi hekima hii na maajabu?

55. Je, huyu si yule mwana wa seremala? Je, mama yake si anaitwa Maria, na ndugu zake si kina Yakobo, Yosefu, Simoni na Yuda?

56. Na dada zake je, si wote wako hapa pamoja nasi? Basi, amepata wapi haya yote?”

57. Basi, wakawa na mashaka naye. Lakini Yesu akawaambia, “Nabii hakosi kuheshimiwa, isipokuwa katika nchi yake na nyumbani mwake!”

58. Kwa hiyo, hakutenda miujiza mingi pale kwa sababu ya kutoamini kwao.