Agano la Kale

Agano Jipya

Hesabu 16:31-44 Biblia Habari Njema (BHN)

31. Mara tu alipomaliza kusema maneno hayo yote, ardhi chini ya Dathani na Abiramu ikafunuka

32. kuwameza watu hao, jamaa zao, pamoja na wafuasi wote wa Kora na mali zao zote.

33. Basi, wao, pamoja na vyote vilivyokuwa vyao wakashuka kuzimu hali wangali hai. Ardhi ikawafunika, wote wakatoweka.

34. Waisraeli wote wengine waliokuwa karibu waliposikia vilio vyao walikimbia wakisema, “Tukimbie, ardhi isije ikatumeza na sisi pia.”

35. Kisha Mwenyezi-Mungu akapeleka moto ukawateketeza wale watu 250 waliokwenda kufukiza ubani.

36. Baada ya hayo, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

37. “Mwambie Eleazari mwana wa kuhani Aroni avitoe hivyo vyetezo penye moto, akautapanye mbali moto uliomo ndani, maana vyetezo hivyo ni vitakatifu.

38. Vimekuwa vitakatifu kwa sababu watu hawa walivileta madhabahuni pa Mwenyezi-Mungu. Basi, vichukue vyetezo vya watu hao waliouawa kwa sababu ya dhambi zao, vifuliwe kuwa vyembamba ili viwe kifuniko cha madhabahu. Hili litakuwa onyo kwa Waisraeli wote.”

39. Basi, kuhani Eleazari alivichukua vyetezo hivyo vya shaba ambavyo vililetwa mbele ya Mwenyezi-Mungu na wale watu walioteketezwa vikafuliwa kuwa kifuniko cha madhabahu.

40. Hili lilikuwa onyo kwa Waisraeli kwamba mtu yeyote ambaye si kuhani, yaani asiye wa ukoo wa Aroni asiende madhabahuni kumfukizia Mwenyezi-Mungu ubani. La sivyo ataangamizwa kama Kora na wafuasi wake. Haya yote yalitendeka kama Mwenyezi-Mungu alivyomwambia Eleazari kwa njia ya Mose.

41. Kesho yake, Waisraeli wote walimnungunikia Mose na Aroni wakisema, “Mmewaua watu wa Mwenyezi-Mungu.”

42. Walipokusanyika mbele ya Mose na Aroni ili kutoa malalamiko yao, waligeuka kuelekea hema la mkutano, wakaona kuwa wingu limeifunika hema na utukufu wa Mwenyezi-Mungu ulikuwa umetokea hapo.

43. Mose na Aroni walikwenda, wakasimama mbele ya hema la mkutano,

44. na Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose,

Kusoma sura kamili Hesabu 16